Thursday 26 May 2016

Silaa adai wafuasi wa Chadema walitishia kuchoma nyumba


ALIYEKUWA mgombea ubunge wa Ukonga, Jerry Silaa (CCM) amedai kuwa wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) walimtishia kuchoma moto nyumba yake wakati wa Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka jana.

Silaa alieleza hayo jana katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, wakati akitoa ushahidi wa kesi ya kupinga matokeo yaliyompa ushindi mbunge wa jimbo hilo, Mwita Waitara (Chadema).

Alitoa ushahidi huo kwa njia ya kiapo baada ya Jaji Fatuma Msengi kutupilia mbali pingamizi la upande wa walalamikiwa waliokuwa wanapinga kupokewa kwa kiapo hicho kwa kuwa kina mapungufu kisheria.

Katika kiapo hicho, Silaa anaeleza kuwa, Oktoba 27 mwaka jana katika kituo cha kujumlishia kura cha Pugu Sekondari, kulikuwa na idadi kubwa ya wapiga kura wa Chadema wakiwa wamesimama mita 20 kutokea usawa wa kituo hicho.

Alidai kuwa wafuasi hao walianza kuwatishia Mawakala na Msimamizi wa Kituo, jambo lililosababisha Polisi washindwe kufanya kitu zaidi ya kuwaonya, ndipo mjibu maombi wa pili na wenzake wakasema hawatopokea matokeo na watachoma moto nyumba yake pamoja na kituo hicho.

Silaa ambaye aliwahi kuwa, Meya wa Manispaa ya Ilala, alidai hadi Oktoba 27, baadhi ya vituo vilikuwa havijakusanya matokeo jambo lililosababisha aandike barua kwenda kwa Msimamizi wa Kituo kuomba mchakato wa kuhesabu kura urudiwe.

No comments: