Thursday 20 July 2017

Rais Magufuli Awataka Wakimbizi kutoka Burundi wajiandae kurejea kwao. ....Amuagiza Waziri wa Mambo ya Ndani kusitisha kuwapa uraia.


SeeBait

Rais John Magufuli amewataka wanachi wenye asili ya urundi waliopo nchini Tanzania wafanye wawezavyo kwa hiari yao warudi kwao wakaijenge nchi wasisingizie kuna vita kwa kuwa Rais wao Pierre Nkurunziza ameshawahakikishia kuwa kuna amani ya kutosha.

Rais Magufuli ametoa kauli hiyo wakati akihutubia wakazi wa wilaya ya Ngara mkoani Kagera katika mkutano wa hadhara uliyofanyika katika viwanja vya Posta baada ya kupokea ugeni kutoka nchini Burundi wa rais huyo pamoja na baraza lake la mawaziri mchana wa leo uliyokuja kwa mazungumzo ya kiuchumi.

"Ndugu zangu warundi mmesikia taarifa iliyotolewa na Rais Nkurunziza anawaomba mrudi kwenye nchi yenu, mkajenge nchi yenu, mkajitafutie maisha. Ni kama wanaotoka Afrika kwenda Itali lakini kuna wakimbizi wamezoea kukimbia tu, sasa kwa sababu Rais ameshawaambia murudi nyumbani sasa mchukue hatua za kurudi nyumbani kwa hiyari wala sisi hatuwafukuzi. 


"Ninafahamu wapo baadhi ya watu ambao hufanya biashara na wakimbizi kwa sababu ndipo wanaotoa vyakula, wanaomba misaada kule nje ya kusema kuna wakimbizi sana na saa zingine wanaelezea hali ambayo haipo", amesema Rais Magufuli.

Pamoja na hayo Rais Magufuli ameendelea kwa kusema "Nimesikia wakimbizi wengine wameahidiwa kwamba mtakuwa mnapewa  elfu kumi kumi wabaki sasa nasema wakawapeni hizo hela mkiwa Burundi.


"Nataka tuelezane ukweli kwasababu tunawajibu wa kulinda amani katika nchi zetu na Mhe. Rais ameshazungumza hapa lakini nchini Tanzania tumekuwa na uzalendo mzuri kwamba wakimbizi wanapokuja muda mwingine tunawapa uraia. Sasa kama wapo watu wanakimbia kule kwa sababu waje tuwape uraia waziri wa mambo ya ndani simamisha zoezi la kuwapa uraia wanaokuja huko".

Aidha, Rais Magufuli ameunga mkono ombi la Rais wa Burundi aliyowataka wananchi wake warundi kwao wakaijege kwa pamoja nchi hiyo kwa kuwa hakuna shida ya aina yoyote katika kipindi hiki.

"Na mimi niwaombe nitoe wito kwa ndugu zangu wa Burundi kwa hiyari yao mimi siwafukuzi ila kwa hiari yao warudi nyumbani na niwapongeze wale laki moja na hamsini elfu waliorudi kwa hiari yao pia niyaombe Mashirika yanayoshughulikia wakimbizi waache kuwahubiri wakimbizi kwamba Burundi kuna matatizo, waanze kuhubiri amani ya kweli kwamba wanao uwezo hawa wakimbizi kwenda Burundi", amesisitiza Rais Magufuli.

Kwa upande mwingine, Rais Magufuli amemthibitishia Rais Nkurunziza kuwa Tanzania itaendelea kutoa ushirikiano mkubwa kwa majirani zake wote waliopo ndani ya Afrika Mashariki ndani ya SADC pamoja na nchi ya Burundi.

No comments: