Friday 1 September 2017

Naibu Waziri wa ardhi azionya Halmashauri zinazotelekeza nyumba NHC


Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabulla amezionya halmashauri nchini ambazo zinaomba kujengewa Nyumba na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) na baada ya Shirika kuwajengea wanazitelekeza.

Naibu Waziri Mabulla ametoa onyo hilo wakati alipofanya ziara Mkoani Shinyanga na kugundua kati ya nyumba 50 zilizojengwa na NHC kwa ajili ya Halmashauri ya Kahama ni nyumba moja pekee iliyonunuliwa, licha ya kuwa halmashauri hiyo ndio iliyoomba kujengewa nyumba hizo.

Katika hatua Nyingine Naibu Waziri huyo ameendelea kuwabana maafisa wa ardhi wasiosimamia ipasavyo makusanyo ya kodi ya pango la ardhi na kuwaagiza maafisa hao wa halmashauri ya Shinyanga kumpatia majina ya wadaiwa sugu 100 wa awali ambao hawajalipa kodi ya pango la ardhi kwa miaka mitano iliyopita ili wafikishwe mahakamani au mali zao zipigwe mnada.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Bibi Zainab Tellack alimwomba Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt. Angeline Mabulla kumsaidia kutatua baadhi ya migogoro ya ardhi inayoukabili mkoa wa Shinyanga kabla ya kuondoka.

Katika ziara hiyo Naibu Waziri alitembelea masijala ya ardhi inayotumika kuhifadhia kumbukumbu na nyaraka za zinazohusu hatimiliki.

No comments: