Thursday 14 March 2013

CHADEMA yalisulubu Bunge

WANASHERIA wameunga mkono msimamo wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na wale wa NCCR- Mageuzi kupinga hatua ya Ofisi ya Bunge kuliagiza Jeshi la Polisi kuwakamata wabunge wake ili wakahojiwe.
 Wakizungumza mwanasheria mashuhuri hapa nchini na wakili wa kujitegemea, Mathew Kakamba, alisema ni kinyume cha sheria na ni matumizi mabaya ya madaraka kwa Ofisi ya Bunge kutumia polisi kuwakamata wabunge katika masuala yanayolihusu Bunge.
Wanasheria hao walitoa maoni yao kuhusiana na mvutano mkubwa wa kisheria uliozuka baina ya CHADEMA na Ofisi ya Bunge ambayo imeagiza kukamatwa kwa wabunge kadhaa wa upinzani ili wakahojiwe na Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge, ambayo CHADEMA wanadai kuwa haipo.
Wakili Kakamba katika maoni yake alisema ni makosa kisheria kutumia nguvu za mhimili mwingine katika kuendesha masuala yanayohusu mhimili wa pili.

“Kuna mgogoro unaojulikana kwa  Watanzania karibu wote kuhusiana na vurugu zilizotokea katika mkutano wa Bunge lililokwisha, na kuvunjwa kwa kamati za kudumu za Bunge.
“Pamoja na kuvunjwa kwa kamati hizo, bado kama sikosei, wajumbe wake hawajateuliwa na kwa maana hiyo, kisheria utendaji wake haujaanza. Kwa lugha nyingine, haziwezi kuitwa kamati rasmi kwa sababu hazina wajumbe,” alisema Wakili Kakamba.
Kauli ya Wakili Kakamba imeungwa mkono na wakili mwingine, Aloyce Komba, ambaye  amekiita kitendo cha Ofisi ya Bunge kutumia polisi kuwakamata wabunge wao wa upinzani kuwa ni udhalilishaji mkubwa na uvunjaji wa haki za binadamu.
Komba anayetoka Kampuni ya Uwakili ya Haki Kwanza, alisema Bunge ni chombo kinachojitegemea na linazo sheria na kanuni zinazopaswa kutumika kumlazimisha mbunge kutimiza agizo la wito.
“Masuala yote ya Bunge yanatakiwa kuendeshwa kibunge bila kutegemea vyombo vingine vya nje, labda tu ikiwa kuna mwingiliano kutoka katika mhimili mwingine.
“Si sahihi kwa spika kutumia polisi kuwakamata wabunge wakati wanazo kanuni na taratibu nzuri tu, na sidhani kama ni utaratibu mzuri na unaolenga kudumisha demokrasia.
“Mbunge akishindwa kufika, kwani hakuna sheria nyingine hata za kuzuiwa kuhudhuria vikao kadhaa vya Bunge, hadi leo wanataka kutumia polisi kuwakamata?” alihoji Komba.
Akizungumzia uhalali wa kamati hizo, Komba ambaye ni mtaalamu wa sheria katika mambo ya utawala, alisema kimsingi hazipo, kwa sababu tangu kuvunjwa kwake na kuundwa nyingine, bado spika hajateua wajumbe wa kamati mpya.
“Hajateua wajumbe wa kamati hizo, na ni sawa kabisa kuwa hazipo. Sasa wanaitwa kuhojiwa na kamati gani? Mtazamo wa kisheria ni kwamba hazipo.
Alikwenda mbali zaidi na kuilaumu Ofisi ya Bunge kwa madai ya kuvunja haki za msingi kwa sababu aliyetendewa kosa ni spika (kiti), anayelalamika ni spika, mteuzi wa kamati ni spika na ushahidi mwingi utatoka kwa spika, hivyo kupingana kabisa na haki za sheria ambazo mlalamikaji hapaswi tena kuwa mwendesha mashitaka.
Hata hivyo, mawakili hao walikubaliana na kuwataka wabunge wote waliopata barua za wito kutoka Ofisi ya Bunge kuitikia na si kukaidi.
“Pamoja na kasoro hizo, kama wameitwa na Ofisi ya Bunge, wanatakiwa kwenda na si kugoma. Huko ndiko mahali pekee wanakotakiwa kuwakosoa hao wakubwa, na hata wanao uwezo wa kukataa kuzungumza hata kama kamati yenyewe ingekuwa hai kisheria,” walisema wanasheria hao.
CHADEMA wagoma
Juzi  Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa alimwagiza Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bungeni kuiandikia barua Ofisi ya Bunge ya kukataa wabunge wake kukamatwa na polisi ama kuhojiwa na kamati waliyodai ni hewa, kwa kuwa zilizokuwapo zilivunjwa na Spika Anne Makinda katika kikao kilichoisha mwezi uliopita.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Dk. Slaa alisema kisheria, kanuni na taratibu za Bunge, kamati ambazo zimeshavunjwa haziwezi kufanya kazi yoyote kwa kuwa ni batili mpaka hapo zitakapoundwa kamati nyingine.
Alilitaka Bunge kurejea kanuni za kudumu za Bunge namba 113 (7), inayozungumzia ukomo wa uhai wa kamati za Bunge, uhai wake unaishia Mkutano wa Kumi wa Bunge ambapo inakuwa ni nusu ya kwanza ya uhai wa Bunge lenyewe.
Dk. Slaa alisema kutokana na kifungu hicho, inaonesha dhahiri kwamba Spika Anne Makinda na wasaidizi wake wana matumizi mabaya ya sheria, kutoifahamu vizuri ama kulewa madaraka, hali ambayo CHADEMA haitakubaliana nao.
Hivyo alisema Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge ambayo ilikuwa chini ya Mbunge wa Mlalo, Brigedia mstaafu Hassan Ngwilizi (CCM), haitawahoji wabunge wake kwa kuwa imekwisha kumaliza kazi yake tangu Februari 8, mwaka huu.
Msimamo wa CHADEMA unakuja zikiwa ni siku mbili tangu Ofisi ya Bunge kupitia Katibu Mkuu, Dk. Thomas Kashililah, itumie Jeshi la Polisi kuwataarifu baadhi ya wabunge wa chama hicho kuwa wanahitajika jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mahojiano na kamati hiyo.
Katibu Mkuu huyo alisema kama wabunge wa CHADEMA wanaitiwa kuhusu vurugu zilizotokea bungeni Februari 4, mwaka huu, tayari zimeshatolewa hukumu yake kwa kuwataja wahusika kuwa ni Tundu Lissu (Singida Mashariki), John Mnyika (Ubungo), Paulina Gekul (Viti Maalumu) na Joshua Nassari ( Arumeru Mashariki).
Alisema katika hukumu hiyo ambayo ilisomwa na Spika Makinda ilikuwa ya upande mmoja wa kamati yenyewe iliyokaliwa na wabunge wa CCM ambao waliwaona wabunge wa CHADEMA pekee ndio waliofanya vurugu huku ikishindwa kuwaita wahusika kwa mahojiano.
Aidha, alisema hata kama kamati ya Brigedia Ngwilizi ingekuwa hai, wabunge wake wasingeitii, kwa kuwa tayari imekwisha kuwahukumu.
Hata hivyo Dk. Slaa alitumia nafasi hiyo kumtaka Spika Makinda kwenda kozi kwa ajili ya kujifunza sheria za kuongoza Bunge kutokana na kushindwa kwake katika kipindi chote alichokalia kiti hicho.
“Nasikia Spika Makinda huwa anasema kuwa niwafundishe wabunge wangu sheria, kanuni na  taratibu za Bunge kwa kuwa nazifahamu vizuri, kwani yeye na wanasheria wake wanafanya nini? Kupoka kwake sheria na taratibu za bungeni ndizo zinazosababisha vurugu?” alihoji Dk. Slaa na kuongeza:
“Nataka nimwambie kwamba wakati nipo bungeni, maspika waliokuwa wakiongoza Bunge akiwamo Samuel Sitta walikuwa wakijua kuongoza, kwa kufuata sheria na kanuni zake na ndiyo maana hakuna vurugu zilizokuwa zikitokea na si yeye.”
Aidha, alisema maspika hao walikuwa wanajua kwamba mabunge yote ya Afrika na yale ambayo Tanzania inaiga kutoka kwao yana sheria na taratibu zinazowaruhusu kushangilia hata kuzomea kwa kutaja chama chao na si hivi ambavyo Spika Makinda anavyofanya.
Lissu anena
Akizungumza kwa niaba ya wenzake, Lissu alisema kwa mujibu wa sheria na kanuni za Kamati ya Haki, Kinga na Maadili ya Bunge, zinamtaka Katibu Mkuu wa Bunge Dk. Kashililah kuandika barua hizo kwa niaba ya Spika Makinda lakini hakufanya hivyo.
Lakini pia Lissua alisema hata barua ya polisi (police message) waliyopewa si taarifa tosha ya kujipeleka wao kuhojiwa bali walipaswa kupelekewa taarifa ya kuitwa kwa ajili ya mahojiano na Bunge.
Kutokana na maelezo hayo Lissu alisema hakuna jambo lililofuatwa kisheria, hivyo hakuna watakayemwona, na alidai kuwa tayari hukumu yao ilishatolewa na Mwenyekiti wa kamati hiyo, Brigedia Ngwilizi Februari 8, mwaka huu.

No comments: