Sunday 21 June 2015

Mwakyembe Ajivunia Kumshauri Vyema Rais Kikwete


WAZIRI wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Dk Harrison Mwakyembe amesema kati ya mambo anayoweza kujivunia wakati wa utawala wa serikali ya awamu ya nne ni kuwa miongoni mwa washauri wazuri wa Rais Jakaya Kikwete.
 
Alisema ni mmoja wa mawaziri wanaomshauri katika kusimamia na kutekeleza mambo ya maendeleo ambayo yamewezesha kuboresha huduma mbalimbali za kijamii.
 
Aidha, amesema ni jambo la kusikitisha kuona kuna watu tena baadhi yao wako ndani ya CCM wanajifanya hawajaona maendeleo ikiwemo kukamilika kwa ujenzi wa barabara za lami zinazounganisha kati ya mkoa mmoja na mwingine, maji, afya, elimu na mingineyo.
 
Alisema, serikali ya awamu ya nne inapaswa kupongezwa kutokana na utendaji wake mzuri katika kubuni, kutekeleza na kufuatilia miradi yote iliyopangwa na hiyo inampa sifa kubwa yeye na kumfanya kuwa miongoni mwa watu wenye uwezo wa kugombea Urais wa Tanzania kupitia CCM.
 
Aliyasema hayo jana mjini Songea wakati akiwashukuru wanachama wa CCM waliomdhamini katika harakati zake za kuomba ridhaa ya CCM ili awe mgombea wake, huku akisisitiza kuwa anajiona ana sifa nyingi, ndiyo maana amejitokeza aweze kuendeleza mema yaliyofanywa na Serikali ya Rais Kikwete.

No comments: