Wednesday 6 July 2016

Rais Magufuli Asalimia Wananchi Baada Ya Kuhutubia Baraza La Iddi .......Ampongeza Mufti wa Tanzania kwa kuwaunganisha waislamu wote

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amempongeza Mufti wa Tanzania Sheikh Aboubakar Zubeir bin Ali kwa juhudi zake za kuwaunganisha waislamu wote na kupanua uwigo wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA) kutoa huduma za kijamii na ameahidi kuwa serikali ya awamu ya tano itaunga mkono juhudi hizo.

Rais Magufuli ameyasema hayo leo tarehe 06 Julai, 2016 wakati akihutubia Baraza la Eid el-Fitr kwa mara ya kwanza tangu achaguliwe kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lililofanyika kitaifa katika viwanja vya Karimejee Jijini Dar es salaam.

Dkt. Magufuli amesema kitendo cha kuwaunganisha waislamu wote  katika Baraza la Eid el-Fitr kinafungua ukurasa mpya na ni moja ya hatua muhimu za kuimarisha amani, umoja na mshikamano miongoni mwa waislamu wa makundi mbalimbali pamoja na watanzania wengine waisio waislamu.

Aidha Rais Magufuli amezungumzia juhudi zinazofanywa na BAKWATA katika kuimarisha taasisi zake zinazotoa huduma za kijamii na kulinda mali zake akisema serikali itahakikisha mali zote za waislamu zinakuwa salama na kwamba wote waliodhulumu mali za waislamu watazirejesha.

Awali akisoma taarifa, Katibu Mkuu wa BAKWATA Alhaji Suleiman Said Lolila amesema BAKWATA inakusudia kupanua huduma za kijamii kwa lengo la kuwahudumia wananchi ikiwemo kujenga chuo kikuu Mkoani Dodoma na pia amempongeza Rais Magufuli kwa juhudi zake za kuondoa umasikini huku akimtaka asikatishwe tamaa na wachache watakaoudhika kwa kuguswa na hatua zinazochukuliwa.

Nae Mufti wa Tanzania Sheikh Aboubakar Zubeir Ali pamoja na kumshukuru Rais Magufuli kwa kuongoza bila ubaguzi amewataka watanzania kuungana na juhudi za serikali kupinga matendo maovu ikiwemo rushwa na ufisadi na pia amelaani ndoa za jinsia moja akisema ni kinyume na maadili ya dini.

Baraza la Eid el-Fitr pia limehudhuriwa na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Rais Mstaafu wa awamu ya pili Alhaji Ali Hassan Mwinyi, mabalozi na wabunge.

Gerson Msigwa

Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU

Dar es salaam

06 Julai, 2016

No comments: