Friday 3 July 2015

ALIYEKUWA KOCHA WA MBEYA CITY ATUA KIMONDO FC

Mwalwisi akisaini mkataba



KOCHA mkuu msaidizi wa zamani wa Mbeya City, Maka Mwalwisi ametua katika klabu ya Kimondo baada ya leo kusaini mkataba wa miaka miwili kuitumikia klabu hiyo inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara (FDL).
Mkurugenzi wa Kimondo FC, Elick Ambakisye, ndiye aliyemsainisha kocha huyo mkataba leo mbele ya waandishi wa habari jijini hapa na kueleza kuwa Mwalwisi ana uwezo mkubwa wa kufundisha mpira baada ya kujiridhisha na kiwango chake akiwa na klabu za City na Panone FC ya Kilimanjaro
Naye Mwalwisi amesema amechukua uamuzi wa kutua katika klabu hiyo ya Mbozi ili kuisaidia kufanya vizuri FDL na kupanda Ligi Kuu msimu ujao.
"Nilikuwa na mkataba wa mwaka mmoja na Panone FC ambao umemalizika na ndiyo maana nimesaini mkataba mpya leo. Nimefurahi kujiunga na Kimondo FC maana ni timu ya nyumbani," amesema Mwalwisi na kuongeza:
"Nina uhakika tutapanda Ligi Kuu ikiwa wachezaji na uongozi tutatimiza majukumu yetu ipasavyo na kushirikiana kwa kila jambo muhimu kwa timu."
Mwalwisi alikuwa msaidizi wa kocha mkuu wa Mbeya City msimu wa 2013/14 wa Ligi Kuu Tanzania Bara walipomaliza nafasi ya tatu kwenye msimamo wa ligi hiyo nyuma ya Yanga na Azam FC.
Msimu uliopita alijiunga na Panone FC iliyoshiriki FDL, lakini haikufanikiwa kupanda Ligi Kuu. Timu za Majimaji ya Songea, African Sports ya Tanga, Mwadui FC ya Shinyanga na Toto Africans ya Mwanza zilipanda Ligi Kuu.

No comments: