Wednesday 25 October 2017

TPA yasema idadi ya meli zinazoingia nchini imeshuka

Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) imesema idadi ya meli zinazoingia nchini imeshuka kutoka 1,200 hadi 1,000 huku mapato yanayotokana na biashara hiyo yakiongezeka.

Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo Mhandisi Deusdedit Kakoko alisema kwamba hata mizigo inayoingia nchini pia imepungua.

Kakoko alilazimika kuyasema hayo wakati akijibu swali liloulizwa na Mbunge wa Kilindi, Omary Kigua ambaye alitaka kupata ufafanuzi wa kuhusu hali ikoje katika biashara ya bandari.

“Kuna speculation (minong’ono) kuwa idadi ya meli zinazoingia nchini zimepungua. Nilitaka kufahamu hali biashara ikoje?”alihoji Kigua.

Kakoko alisema hatua wanazochukua zinalenga ufanisi , tija, gharama wanazotoza na huduma kwa mteja na kwamba kwa kukamilisha mambo hayo kutawezesha meli nyingi kuingia nchini.

“Uchunguzi wetu umejionyesha kuwa unapochukua hatua matokeo yake yanakuwa mbele hizi hatua ambazo tunachukua zinazaa matunda.

Alitaja sababu nyingine ya kupungua kwa meli ni uwezo wa kutia nanga kwa meli ambao hutegemea kina cha maji na kwamba kuna meli nyingi ambazo zinasubiri nje ya gati.

Alisema kina cha maji kuna mahali ni mita saba wakati kwingine ni mita 10.5 na meli nyingi duniani ni kubwa hivyo nyingine kusababisha meli kutofika nchini.

“Kwa hiyo kuna meli zinasubiri siku saba na meli inatengeneza hela ikitembea ikisimama inatumia hela kwasababu ni kama gari, hiyo ndio sababu inayotuathiri lakini sasa tumeanza ujenzi wa kuchimba gati zetu,”alisema.

Alisema sababu nyingine za usalama ambapo kuna baadhi ya watu wamekuwa wakiibiwa hadi betri na kwamba nyingine ni usimamizi wa sera ambapo awali kulikuwa kuna baadhi ya watu wanaleta mizigo hawalipii.

Alisema pia kampeni za masoko zilienda chini licha ya miaka 1960 ilikuwa ni bandarini yenye nguvu.

Mbunge wa Magomeni, Jamal Kassim alisema hoja nyingi za ukaguzi kwa mamlaka hiyo zinatoka na mfumo mbuvu walionao taasisi hiyo.

“Mwenyekiti (Mwenyekiti wa Bodi ya Bandari Profesa Ignas Rubaratuka) ulituambia kuwa mmevuka malengo kutoka Shilingi 632 bilioni hadi 705 bilioni lakini kutokana na mfumo mbovu Serikali wharfag (fedha za mizigo) zikusanywe na TRA ( Mamlaka ya Mapato Nchini),”alisema.

“Mkurugenzi atuambie hizo fedha walizokusanya zinajumuisha pia fedha za wharfag na atumbie pia ukoje huo utaratibu?”alihoji.

Akijibu Mhandisi Kakoko alisema wamerejeshewa Sh 112bilioni ambazo ni mapato yanayotokana na mizigo ya kipindi cha Agostihadi Desemba mwaka jana na kwamba walishazitumia.

Hata hivyo, alisema wanadai Serikali Sh 183 bilioni ambazohazijarejeshwa katika mamlaka hiyo.

“Awali makubaliano kati ya TRA na mamlaka kuwa watakusanya mapato hayo ya mizigo lakini hili lilifutika baada ya sheria ya bandari kufanyiwa marekebisho na kutoa mamlaka kwa TRA kukusanya mapato hayo ya mizigo na kisha kurejeshwa kwa TPA,”alisema.

Akisoma maazimio ya kamati hiyo Mwenyekiti wa Kamati hiyo Kaboyoka aliagiza mamlaka kuwasilisha mpango kazi wa kusimika na kuanza kutumika kwa mfumo wa Tehama katika ofisi ya Katibu wa Bunge.

“Bodi ikamilishe zoezi la uthaminishaji wa mali katika mwaka wa fedha 2017/18,”alisema.

Chanzo Mwananchi.

No comments: