Friday 11 January 2013

Tanesco yaanza kutekeleza bei mpya za kuunganisha umeme




Shirikala Umeme Tanzania (Tanesco) limeanza kutekeleza bei mpya za kuunganisha umeme zilizotangazwa na Waziri wa Nishati na Madini Profesa Sospeter Muhongo, kwamba, zingeanza kutumika mwezi huu. Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, mmoja wa maofisa wa Tanesco Wilaya ya Ilala, alisema kuanzia mwezi huu wameanza kutoza Sh. 320,960 badala ya Sh. 455,000 za hapo awali kwa wateja wanaounganisha umeme moja kwa moja bila kutumia nguzo kwa umbali usiozidi mita 30 mijini. 

Alisema kwa wateja wanaohitaji kuunganishiwa umeme kwa njia moja kwa kutumia nguzo moja, wanatozwa Sh. 515,618 badala ya bei ya awali ya Sh. 1,351,884 za awali.


Ofisa huyo, ambaye hakutaka kutaja jina lake kwa kuwa si msemaji wa shirika hilo, alisema kwa upande wa wateja wanaounganishiwa umeme kwa njia moja na nguzo mbili hutozwa Sh. 454,6454 badala ya Sh. 696,670 za awali.
Katika hotuba yake ya bajeti ya wizara yake kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013, aliyoitoa bungeni, mwaka jana, mjini Dodoma, Waziri Muhongo alisema wizara yake  kupitia Tanesco imedhamiria kupunguza gharama za kuunganisha umeme.
Alisema dhamira hiyo inalenga kutimimiza malengo ya serikali ya kuongeza idadi ya Watanzania wanaotumia nishati hiyo kote nchini kutoka asilimia 18 ya sasa hadi asilimia 30 ifikapo mwaka 2015.
Pia akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mpango huo mwaka jana, Waziri Muhongo aliwahakikishia Watanzania kuwa ifikapo Januari, mwaka huu, wataanza kuunganishiwa nishati hiyo kulingana na gharama za punguzo zilizopangwa na serikali kwa wananchi wanaoishi maeneo ya mijini na vijijini.
Kwa mujibu wa punguzo hilo, wateja watakaojengewa njia moja katika umbali usiozidi mita 30 bila kuhitaji nguzo kwa maeneo ya vijijini, wataunganishwa kwa Sh. 177,000 kutoka ile ya zamani Sh. 455,000 sawa na punguzo la asilimia 61.11 wakati kwa upande wa mijini ni Sh. 320,960 kutoka Sh. 455, 000, ambayo ni sawa na punguzo la asilimia 29.48.
Njia moja na nguzo moja kwa upande wa vijijini, wataunganishiwa kwa Sh. 337,740 kutoka ile ya zamani Sh. 1, 351,884 sawa na punguzo la asilimia 75.02 na mijini 515,618 kutoka ile ya zamani Sh. 1, 351,884 sawa na punguzo la asilimia 61.86.
Kwa watakaohitaji kuunganishiwa umeme wa njia moja na nguzo mbili, watalipa Sh. 454,654 kwa wale wa vijijini ni Sh. 696, 670 kwa wale wa mijini, gharama ambazo kwa mujibu wa Wizara ya Nishati Madini, zitaanza kutumika rasmi kuanzia mwezi huu.
Waziri Muhongo alisema matarajio ya kupunguziwa gharama hizo yanakabiliwa na ukinzani mkubwa baada ya Tanesco kutoa maombi ya kupandisha gharama za umeme kwa asilimia 81.27 ili kufidia hasara ya takriban Sh. bilioni 160 kutokana na gharama za matumizi zinazokadiriwa kufikia Sh. bilioni 250 kuzidi mapato yanayoingizwa katika shirika hilo ya Sh. bilioni 90 kila  mwezi.
CHANZO: NIPASHE

No comments: