Wednesday 21 August 2013

MWANAJESHI WA TANZANIA AFUNGUKA,KAGAME UMEIJENGA NCHI KWA MIAKA,UTAIBOMOA KWA DAKIKA

Kagame, kujenga nchi miaka kuibomoa dakika

 
 Iwapo anatarajia maswahiba wake (Burundi na Uganda) kumsaidia, basi ajue vile vile Tanzania nayo inao marafiki wema ambao nao hawatasita kujitokeza kusaidia.

Tanzania na Rwanda, zimekuwa na uhusiano mzuri kwa muda mrefu, lakini uhusiano huu umeanza kuingia dosari pale Tanzania ilipoamua kuingilia mgogoro wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) pale ilipokitaka kikundi cha M23 kiondoke katika nchi hiyo ya Afrika ya Kati.

Majirani wote wa DRC wanajua kinachoendelea katika nchi hiyo lakini kila mmoja ameamua kukaa kimya. Ni Rais Jakaya Kikwete aliyeamua kuvunja ukimya na kutoa kauli iliyozua chuki baina yake na Rais Kagame wa Rwanda.

Chuki zaidi za Kagame dhidi ya Kikwete zimeibuka pale Tanzania ilipoamua kupeleka majeshi yake ndani ya DRC kwa mapendekezo ya UN kwa ajili ya kulinda amani katika kifungu cha saba, kinachoruhusu kujibu mashambulizi pale askari wa kulinda amani wanaposhambuliwa.

Hiki ndicho chanzo cha Rais Paul Kagame wa Rwanda kuanza kutoa matamshi ya kejeli bila kujielewa dhidi ya Tanzania na rais wake.

Kuna madai kwamba M23 imekuwa ikichukua madini nchini DRC na kuyapeleka Rwanda kwa makubaliano maalumu na Serikali ya Kagame. Kama madai hayo ni kweli, basi ni wazi kuwa M23 inasaidia kwa kiasi kikubwa uchumi wa Rwanda kukua kwa haraka.

Hata hivyo, lawama hizo zote za bure, maana si Tanzania pekee iliyopeleka majeshi kulinda amani DRC, kwani majeshi ya Afrika ya Kusini, Msumbiji na Malawi nayo yapo nchini humo.

Bila shaka Rais Kagame anaona sasa ile njia ya kukuza uchumi wa Rwanda kupitia DRC itakuwa ngumu, hivyo akaona njia pekee ni kupambana na Rais Kikwete bila kujali kuwa mtazamo wake ulikuwa ni kuwasaidia wananchi wa Congo, ambao wanateseka muda mrefu kwa na majeshi ya M23.

Ikumbukwe kuwa kilichomuondoa aliyekuwa Rais wa nchi hiyo, Mobutu Seseseko, ni kikundi cha Banyamulenge kilichofadhiliwa na nchi za Uganda na Uganda pamoja na Marehemu Laurent Kabila, baba yake Rais wa sasa wa Congo, Joseph Kabila, na wanajeshi wa nchi hizo waliokuwa Tanzania muda mrefu.

Marehemu Kabila alikaa kwa muda mfupi sana madarakani na yakajitokeza matatizo kati yake na washirika wake Banyamulenge (Rwanda/Uganda), na mara zikaanza vurugu na hatimaye vita rasmi na kupeleka mashambulizi Goma kuelekea Kinshasa hadi Kabila alipoomba msaada kutoka Zimbabwe na Angola.

Majeshi ya nchi hizo za Angola na Zimbabwe yalifanikiwa kuyarudisha nyuma majeshi ya Rwanda na Uganda ingawa baadaye waasi walifanikiwa kujipenyeza na kumuua Rais Kabila, ingawa walishindwa kumweka kibaraka wao kama walivyo kusudia, na nafasi yake kuchukuliwa na mwanaye Joseph Kabila ambaye naye amekuwa na misimamo isiyoyumbishwa hadi leo.

Historia ya Tanzania tangu enzi za rais wa Kwanza wa Tanzania Mwalimu JuliusNyerere, ilikuwa kulisaidia Bara la Afrika na watu wake kupata amani, na ndicho alichoonekana kufanya Rais Kikwete DRC.

Chokochoko za Kagame wa Rwanda zinafanana na zile za Idd Amin Dadaa wa Uganda mwaka 1978 alipotoa maneno ya kejeli kwa nchi yetu na hatimaye kutuma majeshi yake kuvamia sehemu ya nchi hii kwa madai kuwa ni mali ya Uganda.

Mwalimu Nyerere ambaye alikuwa msimamizi wa amani ya Afrika, alichoshwa na aliyoiita dharau kipindi kile na akatangaza vita dhidi ya Uganda.

Nyerere alipoamua kupigana na Idd Amin alimwambia “War is not a dance” (vita siyo muziki) na ndivyo ilivyokuwa kwani majeshi ya Tanzania yalifanikiwa kuyarudisha nyuma majeshi ya Uganda chini ya rais wao mvamizi, Idd Amin Dadaa.

Namshauri Rais Kagame, kabla ya kuamua kuingia vitani na nchi yetu afanye uchunguzi wa kutosha ili baadaye asije akayajutia maamuzi yake.

Aelewe kuwa Tanzania ni nchi kubwa sana na pia ina idadi kubwa ya wananchi wenye mapenzi na nchi yao ambao hawatakaa kimya na kusubiri aitukane na kuonyesha dharau kwao.

Iwapo anatarajia maswahiba wake (Burundi na Uganda) kumsaidia, basi ajue vile vile Tanzania nayo inao marafiki wema tu ambao nao hawatasita kujitokeza kusaidia.

Kagame akae akijua kuwa, kujenga nchi ni kazi kubwa inayofanywa kwa miaka mingi, lakini kuibomoa ni dakika moja tu.

Asithubutu kuichezea nchi yetu kwani hakuna Mtanzania atakayekaa kimya akimsubiri aivuruge amani yetu.

Mwandishi wa makala haya ni mwanajeshi mstaafu.

No comments: