Wednesday 5 March 2014

HATIMAYE MATATUU YAGOMA NAIROBI


mgomo_matatu_nairobi_7b40f.png
Wakazi wa jiji la Nairobi wakienda makazini kwa miguu asubuhi hii kufuatia mgomo wa matatu.  Picha kwa hisani ya Daily Nation
Na Fadhy Mtanga
WAKAZI wa jiji la Nairobi nchini Kenya wameonja joto ya jiwe asubuhi hii baada ya kulazimika kwenda makazini na maeneo mengine kwa miguu kufuatia mgomo mkubwa wa madereva wa usafiri wa umma, maarufu kama matatu.
Madereva hao waliamua kuifunga barabara ya Thika karibu na daraja la waenda kwa miguu la Pangani. Kisa cha kadhia hiyo ni kuongezeka kwa gharama ya kupaki jijini hapo.
Gazeti la Daily Nation la nchini humo limeripoti kuwa madereva hao waliyaweka magari yao kwenye mzunguko mkubwa wa Donholm na kuwalazimisha wakazi wa jiji hilo kutumia barabara ya Jogoo ili waweze kufika makazini ama maeneo mengine kadri ya mahitaji yao.
Mkuu wa kitengo cha usalama barabarani Nairobi amesema polisi wamefanya jitihada kubwa ili kuweza kuzifungua barabara za Jogoo, Thika na Donholm kufuatia madereva kuweka vizuizi asubuhi ya leo.
Adha hiyo pia imewafanya wakazi kadhaa kuporwa vitu vyao na vibaka huku wakiilalamikia mamlaka husika kwa kuchangia kadhia hiyo.
Chama cha wafanyabiashara jijini hapo, Nairobi Metropolitan Union kimemtaka Gavana kushusha gharama hizo. Waendeshaji hao wa matatu wanataka gharama kwa matatu ya abiria 14 kushushwa hadi shilingi za Kenya 3,650 kutoka shilingi 5,000, huku zile za abiria 41 zikishushwa kutoka shilingi 8,000 hadi 5,000.
Tayari mamlaka za kaunti zimeridhia madai hayo.

No comments: