Friday 17 April 2015

Kesi ya udhalilishaji, Makonda apewa siku saba kujitetea.

kisutu


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam imempa siku saba Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Paul Makonda kuwasilisha utetezi wake kwenye kesi inayomkabili ya kutoa maneno ya udhalilishaji dhidi ya baadhi ya viongozi wa Chama cha Mapinduzi.

Kesi hiyo ilifunguliwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Singida Mgana Msindai na aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam John Guninita wakimtaka Makonda awaombe radhi na kuwalipa kiasi cha shilingi milioni mia moja kila mmoja kwa udhalilishaji huo.

Madai ya Guninita na Msindai yametokana na maneno yanayodaiwa kutolewa na Makonda wakati akiwa Mwenyekiti wa uhamasishaji wa Chipukizi wa CCM kwenye mkutano wake na Waandishi wa Habari ambapo anadaiwa kutoa maneno ya kuwadhalilisha kwa kuwaita wao ni vibaraka wa CCM na kwamba hawafai kuwepo ndani ya chama.

Makonda ambaye hakuwepo mahakamani na kuwakilishwa na wakili wake Peter aliitaka mahakama hiyo kutoa muda zaidi kwa kuwa mteja wake amekabiliwa na shughuli za Serikali.

Katika kesi hiyo Msindai na Guninita wanaotetewa na Wakili Benjamini Mwakagamba wanaiomba mahakama iamuru pamoja na mambo mengine itoe zuio la kudumu kwa Makonda asizungumze  tena maneno ya kashfa wala kuyasambaza kama alivyofanya awali.

Katika hati ya mashtaka ya Mkonda imeonesha kupokea barua ya madai kutoka kwa Guninita na Msindai iliyomtaka kuwaomba msamaha kwa maneno yaliyotoa dhidi yao ambapo aliwajibu kamwe hatawaomba radhi na kwamba alifanya hivyo kwa nafasi yake ndani ya chama kwa kufuata Katiba, Muongozo na Kanuni.

Wakati huo huo Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo wilaya ya Ilala imeyafikisha mbele ya baraza la usuluhishi la ardhi Makampuni 123 yakiwemo ya umma, binafsi na mashirika ya dini kwa kukwepa kulipa kodi ya pango.

Mwenyekiti wa baraza la usuluhishi la ardhi wilaya ya Ilala Yose Mlyambana amesema kulingana na baadhi ya kesi ambazo tayari wamekwishazisoma hadi sasa juma ya shilingi milioni 50 zinakadiwa kupotea.

Miongoni mwa makampuni yaliyofunguliwa kesi kwenye Baraza hilo la Ardhi na Nyumba wilaya ya Ilala ni Mmiliki wa Kampuni St. Mary’s International School, Murzah Oil Mills Limited, Oil Com, Highland Estate na Jessa Industries na S. H Amon.

No comments: