Tuesday 30 June 2015

Serikali yatakiwa kufunga vyuo vikuu visivyokuwa na viwango nchini.



Sakata la migogoro ya vyuo vikuu vinavyodaiwa kutokuwa na usajili au kutokidhi viwango vinavyotakiwa limeibuka tena bungeni ambapo baadhi ya wabunge wameitaka serikali kuvifungia  kwani licha ya kuwapotezea muda wanafunzi vinawatia hasara wazazi na serikali inayotoa mikopo kwa wanafunzi hao.
Hayo yameibuka bungeni mjini Dodoma wakati wa kipindi cha maswali na majibu ambapo baadhi ya wabunge wameihoji serikali kwa nini inaendelea kuviachia vyuo hivyo viendelea kutoa huduma ambayo mwisho wa siku inaitia hasara taifa kikiwemo chuo cha st joseph ambacho kinadaiwa kutokuwa na usajili na chuo cha kampala ambacho hakina usajili wa bodi ya famasia.
 
Akijibu maswali hayo naibu waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi Mh Janesta Muhagama mbali na kukiri uwepo wa vyuo ambavyo havifuati taratibu za nchi amelihakikishia bunge hilo kuwa serikali inafanya utafiti wa kina kwa kushirikiana na kamati ya huduma za jamii na kuongeza kuwa vyuo vitakavyobainika hatua zitachukuliwa.
 
Suala la uhaba wa nishati ya mafuta nchini nalo likaibuka ambapo mbunge wa Ubungo John Mnyika amewasilisha hoja ya dharura bungeni ili wabunge waweze kujadili suala hilo liweze kupatiwa ufumbuzi wa haraka kabla madhara hayajawa makubwa.
 
Hata hivyo hoja hiyo haikuweza kuendelea kujadiliwa na wabunge baada ya naibu spika Mh Jobu Ndugai kuwahidi wabunge hao kuwa endapo tatizo hilo halitapatiwa ufumbuzi mapema mjadala utaruhisiwa huku serikali ikikanusha kutokuwepo kwa uhaba wa mafuta na kwamba yapo ya kutosha, na kutoa onyo kwa wenye vituo vya mafuta ambao wameyaficha kwa madai ya kusubiri bei mpya.

No comments: