Wednesday 20 September 2017

Polisi Dar yakamata ‘Wasiojulikana’ watano


Jeshi la polisi kanda maalum ya Dar es salaam limetangaza kuwakamata watu watano ambao wamekiri kufanya uhalifu na kuvunja katika ofisi ya Mawakili ya Prime Atorneys iliyopo katika jengo la Prime house, Mtaa wa Tambaza, Upanga jijini Dar es Salaam.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amefunguka na kusema kuwa jeshi la polisi limeweza kuwakamata watu hao ambao mwanzo baadhi ya wananchi walikuwa wakisema watu wasiojulikana ambao walifanya uhalifu huo na kudai wamekiri kuhusika na uvunjaji wa ofisi hiyo na kuiba.

"Kutokana na msako mkali jeshi la polisi limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa watano kuhusiana na kesi ya uvunjaji wa ofisi ya Mawakili ya Prime Atorneys mnamo Septemba 12, 2017 jeshi la polisi lilipokea taarifa ya kuvunjwa kwa ofisi ya mawakili hao ambapo wahalifu hao walifanikiwa kuvunja na kuiba kasiki iliyokuwa na pesa milioni tatu laki saba, waliiba kompyuta mpakato mbili pamoja na nyaraka mbalimbali za ofisi hiyo na wateja" alisema Lazaro Mambosasa

Aidha Kamanda Mambosasa aliendelea kusema kuwa kutokana na msako mkali uliofanywa na jeshi la polisi uliweza kuwakamata watu watano ambao waliwataja kuwa ni pamoja na "Said Idrisa Salehe (47), Mustapha Ibrahim Said (35), Somvi M Somvi (52), Imani Bago Mhina (36) na mshtakiwa na watano ni Husein Hajib Suleman (45) baada ya mahojiano na watuhumiwa hao wote wamekiri kuhusika na tukio hilo na kuonyesha Kasiki la fedha pamoja na mitungi mitatu ya gas iliyotumika kuvunja ofisi hiyo" alisema Mambosasa

Aidha Mambosasa amewataka Watanzania pamoja na viongozi mbalimbali kuwa wavumilivu pundu tukio linapotokea na kutoa nafasi kwa jeshi la polisi kuweza kufanya uchunguzi na upelelezi wake wa kina kuwapata wahalifu wanaokuwa wamehusika kwenye matukio hayo.

"Kwa hiyo masihara mengine yanayofanywa na Watanzania yanalenga kupotosha ukweli lakini pia wanajaribu kuingilia upelelezi wa polisi ili ukweli usijulikane sote sasa tunashuhuda tulianza kwa kutowafahamu mashuhuda lakini upelelezi wa kina umefanyika na tumewapata kwa majina na wao wenyewe wamekiri kufanya matukio hayo, sasa nimualike aliyekuwa akipotisha Watanzania kwa nguvu kuwa aliyetenda kosa hilo hajulikani aje sasa atueleze kuwa na yeye ni miongoni mwa waliotenda makosa hayo kwa sababu tayari hawa wapo na wamekiri kufanya makosa hayo" alisisitiza Mambosasa

No comments: