Friday 22 September 2017

Wanasheria Uingereza Wamwandikia Barua Rais Magufuli Sakata la Tundu Lissu


SeeBait
Taasisi tatu za juu za wanasheria za Uingereza zimeungana na kumwandikia barua ya wazi Rais John Magufuli zikiomba mamlaka kufanya uchunguzi wa kina juu ya tukio la kupigwa risasi kwa Lissu na kumfutia kesi zote zinazomkabili ambazo zimekosa ushahidi wa kutosha.

Barua hiyo imeandikwa juzi na kusainiwa na vigogo wa Chama cha Mawakili Uingereza (LS), Kamati ya Haki za Binadamu ya Wanasheria Uingereza (BHRC) na Baraza la Wanasheria (BC).

Vigogo hao, Rais wa LS, Joe Egan; Mwenyekiti wa BHRC Andrew Langdon na Mwenyekiti wa BC, Kirsty Brimelow wamesema wanaguswa na matukio yanayoendelea dhidi ya Lissu ikiwamo ya matukio ya kukamatwa na polisi na kufunguliwa mashtaka mara kwa mara huku pia ikiorodhesha matukio mengine ya kihalifu yaliyowakumba wanasheria wengine likiwamo la kulipuliwa ofisi ya kampuni ya uwakili ya Immma ya jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

Pia, wamesema wameguswa na vitisho dhidi ya TLS kikiwemo cha kukifuta chama hicho kilichotolewa na Dk Harisson Mwakyembe mapema Februari wakati akiwa Waziri wa Katiba na Sheria iwapo ingeendelea kujihusisha na “uanaharakati wa kisiasa.”

Kutokana na mwenendo wa matukio hayo, barua hiyo inaomba ufanyike uchunguzi wa kina na huru utakaoibua ukweli juu ya kupigwa risasi kwa Lissu na matukio mengine ya uhalifu yaliyowakumba wanataaluma wengine wa sheria na kuwachukulia hatua wote wanaohusika kwa mujibu wa sheria na taratibu za kimataifa.

“Tunazisihi mamlaka kumfutia mashtaka yote yanayomkabili Lissu vinginevyo kuwe na ushahidi wa kutosha na uwe wa wazi na kuwe na fursa ya kukata rufaa,” inasomeka sehemu ya barua hiyo na kuongeza;

“Tunaisihi Tanzania kuheshimu matakwa ya kimataifa, iwalinde wanasheria ili kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao vyema bila vitisho, vikwazo, unyanyasaji wala kuingiliwa majukumu yao.”

No comments: