Saturday 13 July 2013

HOFU YATANDA KYELA KUTOKANA NA KASI YA KIPINDUPINDU KUONGEZEKA.



Juhudi za kuudhibiti ugonjwa wa Kipindupindu Wilayani Kyela huenda ukagonga mwamba kutokana na milundikano ya taka ngumu kuongezeka siku hadi siku kama inavyoonekana katika picha zikionesha ndani na nje ya soko kuu  huku kukiwa na hofu kuwa ugonjwa huo utazidi kuenea kama juhudi za haraka hazitachukuliwa.

MBALI na maambukizi ya Ugonjwa wa Kipindupindu kushika kasi Wilayani Kyela Mbeya  kutoka wagonjwa 39 wiki iliyopita hadi kufikia wagonjwa 75 kwa takwimu za jana hali ya mazingira ndani ya Wilaya hiyo hasa Mamlaka ya Mji mdogo wa Kyela wazidi kuwa mchafu kutokana na kukithiri kwa mlundikano wa taka ngumu  kuzidi kuongezeka siku hadi siku.
 
Baadhi ya wakazi wa mji wa Kyela wametoa malalamiko hayo jana kwa Afisa mtendaji mkuu wa mamlaka ya mji mdogo baada ya kuona hali ni tete kutokana na kuongezeka  kwa ugonjwa wa kipindupindu huku Serikali ikishindwa kuuweka mji wa Kyela katika hali ya usafi kitu ambacho kinawapa hofu juu ya kuudhibiti ugonjwa huo.
 
Wafanyabiashara katika soko kuu la Kyela kwa upande wao wameshangazwa na kitendo cha mamlaka hiyo ya mji mdogo  kushindwa kutoa taka ngumu zilizojaa kila kona ya soko na nje ya soko hilo bila kuziondoa huku wakiendelea kutozwa ushuru.
 
Wamewataka viongozi hao kuondoa taka hizo ili kurudisha hadhi ya mji wa Kyela na wao waweze kuona fedha zao wanazozitoa kwa ajili ya ushuru wa uzoaji wa taka ngumu ukifanya kazi.
 
Afisa mtendaji mkuu wa mamlaka ya mji wa kyela Teo Samwel mbali na kukiri kuwepo na hali hiyo pia alisema kuwa tatizo ni gali linalotumika kubeba taka limeharibika na lipo katika matengenezo wataziondoa taka hizo pindi matengenezo ya gali hilo yatakapokamilika.
 
Naye  Mganga mkuu wa Wilaya ya Kyela Apasalia Lumisha alitaja ongezeko la wagonjwa wa Kipindupindu kuwa ni 75 mpaka hivi sasa na waliopoteza maisha kufuatia kukumbwa na ugonjwa huo ni watu watatu.
 
Alisema kuwa kufuatia hali hiyo halmashauri ya wilaya imetenga eneo la uwanja wa Mwakangale mjini Kyela na kujenga mahema matano ya kuanzia kama kambi kuu ya kuhifadhi wagonjwa hao wa kipindupindu na kuwa wote waliolazwa katika hospitali ya wilaya watahamishiwa katika uwanja huo.
 
Alisema kuwa bado jamii inapuuzia juu ya mlipuko huo wa kipindupindu na ndiyo maana kasi hiyo imeendelea na kuwa anakazia amri yake aliyoitoa juzi ya kukataza mikusanyiko mbalimbali ya watu isiyo rasmi,minada na sherehe mbalimbali sambamba na biashara ya vyakula na vilabu vyote vinavyouza pombe za kienyeji
 
Pia mkuu huyo wa wilaya ameagiza wafanyabiashara kuacha kupeleka biashara ya vyakula katika shule zote za msingi na sekondari kwa kipindi hiki ambacho shule zimefunguliwa mpaka pale watakapo tangaziwa na kupewa ruhusa.
 
Ugonjwa huo wa kipindupindu umezidi kuenea maeneo mbalimbali ya wilaya Kyela ambapo awali kata sita za  Kajunjumele,Bujonde,Ikolo,Katumbasongwe na Kyela mjini ndizo zilikuwa na wagonjwa hao lakini sasa hata kata ya Ipande mgonjwa mmoja ametambulika na kupoteza maisha.
 
Aliongeza kuwa kumekuwepo na ugumu kwa wananchi kupokea ushauri kuhusu nanma ya kujikinga na ugonjwa huo ambao unakwepeka na kuwa bado wanaendelea kutembelea kila Kata ndani ya wilaya  ili kuzidi kutoa elimu na namna ya kujikunga na maambukizi ya ugonjwa huo ikiwa ni pamoja na kugawa dawa za kutibu maji (Water guard).
 Na Ibrahim Yassin, Kyela
 

No comments: