Sunday 17 November 2013

TANESCO: MIKOA 14 KUBABILIWA NA UPUNGUFU WA UMEME


    tanesco 8ad7d
SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) limesema utakuwapo upungufu wa umeme katika mikoa iliyounganishwa na gridi ya taifa kutokana na matengenezo ya visima vya gesi vinavyofanywa na Kampuni ya Pan Afrika. (HM)
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam Meneja Uhusiano wa TANESCO, Badra Masoud alisema lengo la matengenezo hayo ni kuboresha upatikanaji wa gesi ya kutosha kutoka katika kisiwa cha Songosongo mkoani Lindi.
"Katika kipindi hiki cha matengenezo tutaongeza uzalishaji wa mafuta na maji na ile mitambo ambayo haitaweza kwenda kwenye mafuta tutaisitisha wananchi waweze kupata huduma hii muhimu.
"Haya ni matengenezo ambayo hayaepukiki kwani lengo lake ni kuboresha miundombini hii na wananchi wasije wakaona kuwa tatizo hili limepangwa kwa makusudu kwa kuwakosesha umeme,"alisema.
Alisema matengenezo hayo yataanza Novemba 16 hadi Novemba 26 mwaka huu na mikoa ambayo itaathirika ni Dar es Salaam, Pwani, Dodoma, Shinyanga, Morogoro, Arusha, Tanga, Mwanza, Mbeya, Iringa, Tabora, Singida, Manyara na Zanzibar.
Amewatahadharisha wananchi kuepuka kuacha vifaa vya umeme wazi wakati wa tatizo la umeme kuepuka kuunguliwa na vyombo vyao vya umeme, pia watumie vifaa maalmu vya kulinda vyombo vya umeme.
"Mwaka huu umeme utakatika mara kwa mara kwa sababu ya maboresho ya ufundi kwa vile tumegundua Tanzania bila umeme haiwezi kuendelea,"alisema. Chanzo: Mtanzania

No comments: