Monday 29 June 2015

Wagombea Urais Wafika 42 CCM


MWANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Banda Sonoko, jana amechukua fomu ya kuomba kuteuliwa na chama hicho ili kugombea urais kwenye Uchaguzi Mkuu ujao akiwa ni mgombea wa 42.

Baada ya kuchukua fomu hiyo jana, Sonoko alisema kama chama hicho kitampitisha kuwa mgombea urais katika Uchaguzi Mkuu ujao na kushinda, moja ya vipaumbele vyake ni pamoja na kuzingatia misingi imara ya ilani ya 2005 pamoja na kuondoa umaskini kwa Watanzania.

Sonoko amewahi kushika nyadhifa mbalimbali ikiwemo ya Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali ya Temeke ambapo katika kampeni zake za kusaka urais atatumia kauli mbiu inayosema "Kutokomeza Umaskini".

Alisema akiingia Ikulu, atawatimizia Watanzania mahitaji mbalimbali ambayo wameyakosa muda mrefu ambapo yeye ana sifa zote za kuwa rais ndio maana ameamua kuchukua fomu.

Aliongeza kuwa atahakikisha nchi inaendeshwa kwa kodi za wananchi si misaada kutoka nchi wahisani ambapo wanawake watawezeshwa katika mambo mbalimbali na kupewa nyadhifa kwenye vyombo vya maamuzi pamoja na vijana.

Sonoko alisema Serikali ambayo ataiongoza itasimamia haki, kupinga vitendo vya utoaji na upokeaji rushwa hasa Mahakamani ambapo kesi zitakuwa zikiendeshwa kwa muda maalumu, kurudisha viwanda, kuinua kilimo na kuboresha miundombinu.

"Nitahakikisha kila Wilaya inakuwa na sehemu yake ya kuegesha magari, kuongeza ajira na kuwasaidia vijana," alisema na kuongeza kuwa, hadi Julai mosi, mwaka huu, atakuwa amekamilisha taratibu za kupata wadhamini 450 katika mikoa 15.

No comments: